Sunday, July 14, 2013

IELEWE SAIKOLOJIA YA WATOTO .........KATIKA JITAMBUE KISAIKOLOJIA NA CHRIS MAUKI


Jinsi ya kuwaelewa bayana watoto na kuboresha ukaribu baina yetu na wao.

1.         Faida/Manufaa ya Kuwa karibu na Watoto:
            Yako manufaa na faida nyingi kwa sisi kuwa karibu na watoto.
Watoto wanaweza kukufanya kuhisi umuhimu fulani na kuhitajika wakati wote na wao.  Mara zote hukubali madhaifu yetu na kuyashangilia yale wanayoyapenda kutoka kwetu.

Ni watu wa kusamehe kwa urahisi sana, kamwe hawawezi kuficha wanachofikiri au kukihisi, uwazi wao huu ni faida kwetu ingawa mara nyingine watu wazima wengine hukasirika.  Ukweli ni kwamba uwazi wao kwetu haumaanishi kutuumiza au kutuumbua.

Ni faida kubwa kwetu pale tunapoona ukaribu wetu na mtoto au watoto fulani unabadilisha maisha au tabia zao.  Kupitia jitihada zako watoto wanaweza kujifunza kujitegemea, ushirikiano, mambo ya afya, kupendana n.k.

Watoto wa leo wengi wanaishi au kupitia katika familia zenye mazingira magumu sana, mfano: Familia zenye ulevi, unyanyasani, talaka na kutengana, matatizo ya kiuchumi.  Watoto hawa wanahitaji kutiwa moyo kuliko wale wenye hali njema.  Utajisikia faraja sana pale utakaposaidia kwa namna moja au nyingine mtoto mmoja kuifikia hatima yake vema.

Kuwa karibu na watoto hutuwezesha kubakia ujana hasa katika fikra zetu.  Hali ya kuutazama ulimwengu na maisha kama mtoto anavyotazama hutupa kupunguza au kuondokana na misongo ya mawazo ya maisha.  Tunajikuta tunafurahia kila kitu kama vile watoto wafanyavyo, hapa tunasema “Yatazame maisha katika jicho la mtoto”.

Kwa kuwa karibu na watoto tunapata nafasi ya kutambua vipawa vyetu, hasa vile vilivyojificha na kuviweka katika utendaji kwa manufaa ya watoto, sisi wenyewe, na jamii nzima kwa ujumla.

Hata kama ukaribu na watoto ilikuwa ni ngumu kwako, taratibu utakapojaribu itafukua upendo wa kweli toka moyoni mwako na mara utatamani kuwa karibu na kujifunza kutoka kwao.

2.         Changamoto Zilizopo:
·      Kwa wengi, inaonekana kabisa kuwa, kuwa karibu na watoto mara nyingi huchosha hisia, akili, mwili na hata kusababisha msongo wa mawazo mara nyingine.  Hii huwa ngumu zaidi pale ambapo huna upendo wa dhati kwa watoto.

·      Baadhi ya mahitaji au misaada ambayo hatuna budi kuifanya tunapokuwa na watoto hutupa changamoto na wengine huona ni kinyaa au uchafu.

·      Mara nyingine yaweza kuwa rahisi kuambukiza baadhi ya magonjwa madogo madogo kama mafua, kikohozi, ndui n.k. au wewe kuwaambukiza wao pia.

·      Mara nyingine kuwa karibu na wato hutugharimu.  Ziko nyakati ambazo watataka kitu ambacho kinahitaji kununuliwa kwa fedha, au waweza kulazimika kutumia muda wako kufanya matakwa yao.

·      Ziko nyakati watoto hupitia magumu katika familia zao na hali hii huweza kuathiri tabia au hisia zao nahii kuwa changamoto kwa yule aliyekaribu nao.  Mfano magonjwa ya muda mrefu kwa mzazi au wazazi, vifo, kutengana kwa wazazi n.k. hivi vyote vyaweza kuathiri hisia na tabia za mtoto.

Mambo yatakayo tuwezesha kuboresha ukaribu / urafiki baina yetu na watoto:

1.         Kuwakubali na kuwapenda watoto (Appreciation)
Ni ngumu kabisa kuwa karibu na watoto na kutafuta kukubalika nao pasipo kwanza kuwakubali.  Mawasiliano yako na wao yanatakiwa kuwa ya kiwango cha juu kuliko yale unayofanya na watu wazima.  Kama ni mzazi, tamani au tafuta kuutumia muda unapokuwa na watoto vizuri.  Wape muda na wewe kadri inavyowezekana.

Shiriki nao katika baadhi ya yale wanayoyafanya.  Washirikishe pia katika yale unayodhani watapenda kuona ukiyafanya.  Usiwaangalie tu au kuwaacha wakutazame ukifanya.  Kumpakata mtoto wakati wa hadithi ni mfano wa kushiriki nae.  Hii hujenga mahusiano mazuri sana kwao.

2.         Kuwa tayari kutumia nguvu zetu au nishati yetu ya mwili kwa ajili yao
Watoto huwa na nishati au nguvu nyingi katika vile wanavyovifanya.  Hali kadhalika mtu anayetamani kuwa karibu nao ni lazima awe tayari kutumia nguvu zake katika kushiriki nao.  Mfano, watapenda kukimbizana, watapenda kuruka, au kutembea haraka na michezo mingine mingi.

3.         Kuwa na hali nzuri ya utu (Sense of humor)
Hali hii huwafanya watoto kukuona wewe ni sawa nao.  Watoto hupenda sana pale unapokuwa tayari kucheka na kuwa na hisia kama walizonazo.
Najua unahitaji muda wa kuwaza juu ya biashara au kazi zako, na watoto nao kwa upande mwingine wanataka muda ambao hutawaza yalio yako bali yaliyo yao tu.

Mara nyingine, watoto hufanya vitu vya kuchekesha, tunachotakiwa ni kucheka nao na sio kuwacheka.  Hii itaepusha kuwaumiza moyo.

4.         Uvumilifu (Patience)
Uvumilivu ni muhimu sana kwa yeyote anayetaka kuwa karibu na watoto.  Watoto hufanya makosa mengi, na pia ni wataratibu katika kufanya mambo maana ujuzi wao bado ni mdogo.  Kwanza ndio wanajifunza kujitawala na kufuata maelekezo na pia wanahitaji kukumbushwa mara kwa mara.  Ni wakati wa kuulizwa maswali mengi na ya marudio, hata yale yasiyo muafaka.

5.         Kuwa na huruma (Compassion)
Huruma kwa watoto huambatana na uvumilivu.  Mtu mwenye huruma ni yule anayetambua pale mwenzake anapokuwa na tatizo au uhitaji na yuko tayari kutoa msaada.  Watoto humwitaji mtu anayewaelewa na kujali mahitaji yao.  Vipo vitu ambavyo vyaweza kuonekana vidogo na vya kawaida kwetu, kumbe kwa watoto ni vikubwa na vyenye kuwaogopesha sana.  Tunategemea huruma na kujali kwako kutaongezeka hasa kwa wale watoto wenye matatizo au uhitaji mkubwa mfano: watoto wenye magonjwa ya kudumu, ulemavu au matatizo ya kifamilia.

6.         Kuwa mtu unayekubali mabadiliko (Be flexible)
Watoto wako tofauti sana na huwezi kuwa tabiri, mara nyingine watataka kitu fulani na mara hubadilika.  Hawana muda wa kufikiri athari au usumbufu wa kubadilika au kubadilisha maamuzi yao.  Kwa sababu ni vigumu kufahamu ni nini kitajiri kwa mtoto baada ya muda mfupi ujao basi ni lazima tuwe tayari kubadilika.  Pasipo hili basi utakuwa na wakati mgumu sana kuwa rafiki wa watoto.

7.         Kuwa Mgunduzi (Be creative)
Mtu mwenye mawazo na fikra za kigunduzi atapata urahisi sana katika kuwa rafiki wa watoto.  Jaribu kuwa mpya kwa watoto kila mara,  sio kila kitu unachofanya kwao kiwe ni kile kile siku zote.  Amsha hamasa yao kwa vitu, mambo au mawazo mapya mawakati wote.  Watoto hawapendi kufanya kitu fulani kwa njia au mfumo uleule kila wakati.

8.         Kuwa mtu wa watu na mpenda watu (Be sociable)
Watoto huwa wanatusoma sana, pale unapojaribu kuwa mwema kwao, kucheka nao na kuwa karibu nao na wakati hauko hivyo kwa wengine ndani au nje ya familia yako unawafanya wasikuelewe na taratibu huanza kukuhofu.
Waruhusu wakuone ukiwa halisi, hususani unapohusiana na wao pamoja na wengine pia.
Wazazi au mzazi anayependa kujitenga na kuwa mpweke hupata shida sana katika kuwafanya watoto kuwa karibu nae.

9.         Maanisha na ujitoe kwao (Be committed)
Wakati unapoamua kufanya kitu na watoto au mtoto, basi maanisha.  Usiwe na vitu vingi wakati mmoja.  Wape nafasi yao na iwe yao peke yao.
Jitoe kufanya vema uwezavyo katika kuhakikisha unawajali na kuwafurahisha watoto.  Watoto pia hufurahi sana pale wanapoona umetoa moyo wako wote kwa ajili yao. Kama umeamua kuanza kitu nao basi malizia, usikiachie katikati.
Kama unajua au kuhisi kwamba hutomaanisha katika lile unalolifanya ukiwa nao basi ni bora uache mpaka pale utakapojiona kuwa utamaanisha.


Imeandaliwa na:
Chris Mauki
Mtaalamu wa mahusiano na ushauri wa kisaikolojia
University of Dar es salaam

USIKOSE KUANGALIA MFULULIZO WA VIPINDI VYA KISAIKOLOJIA KILA JUMAPILI SAA MOJA JIONI DTV

No comments:

Post a Comment