Tuesday, March 5, 2013

Tanesco wanachelea kutangaza mgao wa umeme?

Matokeo yake ni kuzidi kudidimia kwa uchumi kutokana na mgao huo kuathiri shughuli nyingi za kibiashara na sekta nyingine nyingi zinazochangia pato la taifa. Hii ni baada ya Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo kutangaza mwaka jana kwamba mgao wa umeme hapa nchini ungekuwa jambo la historia.
Lakini kwa muda mrefu sasa maswali yamekuwa yakiulizwa kuhusu kukatika kwa umeme mara kwa mara. Kwa miaka mingi sasa Tanesco imekuwa ikitoa visingizio vinavyojirudia na kuonekana vimetolewa mahsusi kuwaghilibu wananchi.
Visingizio hivyo ni pamoja na kukata miti kwenye njia za nyaya za umeme, kubadilisha nguzo zilizooza, kubadilisha au kukarabati transfoma.
Kukataa kuwafahamisha wananchi kuhusu kuwapo kwa mgao na sababu zinazosababisha mgao huo kumewakwaza wananchi, kwa maana ya kutoweza kujipanga vizuri katika shughuli zao mashuleni, vyuoni, majumbani, maofisini, viwandani na katika biashara mbalimbali kama saluni, mabucha na magereji.
Shughuli hizo zimekuwa zikivurugika kutokana na Tanesco kutoweka ratiba ya mgao wa umeme ili wadau wapange shughuli zao kutokana na ratiba hiyo.
Waswahili waliposema mficha maradhi kifo humuumbua, walipatia kabisa usemi huo, kwani Tanesco ambayo imekuwa ikificha matatizo yake na kutoa visingizio lukuki, jana ilitoka mafichoni na kutangaza kwamba inakabiliwa na hali mbaya  kifedha, ikiwa ni pamoja na kulemewa na madeni.
Hatua hiyo ya Tanesco haikuwashangaza wengi.
Sisi tumekuwa miongoni mwa wengi ambao tumekuwa tukisema  shirika hilo livunjwe na kusukwa upya kutokana na muundo wake kutoweza kuleta ufanisi, huku likikwamishwa na vitendo vya ufisadi na hujuma za viongozi na wafanyakazi.
Ni siri iliyo wazi sasa kwamba hali mbaya kifedha imesababisha makampuni yanayozalisha umeme kutishia kusitisha uzalishaji umeme. Tanesco haikopesheki na ndiyo maana ilikosa dhamana ya kukopa benki Sh408 bilioni mwaka jana na sasa inategemea ruzuku ya Serikali. 
Makampuni yanayozalisha umeme yanaidai Tanesco Sh5.4 bilioni kila siku wakati shirika hilo linakusanya Sh2 bilioni tu kwa siku.
Hiyo ndiyo hali halisi ya Tanesco ambayo imekuwa ikiendesha shughuli zake kwa kupandisha bei ya umeme kila mwaka. Serikali sasa imelikatalia kupandisha bei ya umeme. Je, shirika hili lina uhalali wa kuendelea kuwapo? chanzo gazeti Mwananchi

No comments:

Post a Comment